Maji ni rasilimali muhimu kwa maisha ya viumbe vyote na mendeleo ya kiuchumi na kijamii. Kiwango cha maendeleo ya jamii yoyote, ubora wa afya na wa mazingira vinategemea kuwepo kwa maji yakutosha na yenye ubora unaotakiwa. Wingi wa maji yanayofaa kwa matumizi mbalimbali una kikomo. Kutokana na ukomo wa wingi wa maji yenye ubora na umuhimu wake kwa maisha ya kila siku, usimamizi na utunzaji wake lazima uzingatie uwiano wa matumizi yote kwa ujumla wake.
Huduma ya majisafi Mkoa wa Dar es Salaam hutolewa na Mamlaka ya Maji ya Mjini Dar es Salaam (DAWASA) ambayo imekodisha shughuli za utoaji huduma kwa Kampuni ya DAWASCO kwa Mkataba wa miaka 13 (lease agreement).Aidha kwa maeneo ambayo hayajafikiwa na mtandao rasmi wa DAWASA, huduma ya maji hutolewa na Kamati za maji za Jamii, Kamati za maji za Serikali za Mitaa, Jumuia za Watumia maji, Vikundi vya Kijamii, Taasisi za Umma, Taasisi za Majeshi na Watu binafsi. Hatua hizi ni za muda na dharura katika kukabiliana na uhaba wa maji.
Kulingana na Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012, Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa na wakazi wapatao milioni 4.5, idadi hiyo kwa mwaka 2016 inakadiriwa kufikia milioni 5.5. Vyanzo vikuu vya maji ni Mto Ruvu, Mto Kizinga pamoja na maji chini ya ardhi.
Mahitaji ya maji kwa wakazi wa Dar es Salaam ni wastani wa lita milioni 544 kwa siku ambapo uwezo wa uzalishaji ni lita milioni 504 kwa siku. Maji yanayozalishwa yanakidhi mahitaji kwa asilimia 72 kwa wastani wa saa 16 kwa siku. Maeneo yasiyohudumiwa na Mtandao wa DAWASA hupata maji kutoka Miradi inayoendeshwa na Taasisi, Sekta binafsi na Jumuia za Watumia maji kwa usimamizi wa Halmashauri za Manispaa na DAWASA. Chanzo kikubwa cha maji haya ni visima. Hadi kufikia mwezi Juni, 2017 kulikuwa na takribani visima virefu 1,171 vya jamii, visima 147 vya DAWASA na visima 600 vya Taasisi na watu binafsi. Maji yanayozalishwa na visima vya Taasisi na watu binafsi yanafikia lita za ujazo milioni 53 kwa siku ambapo yanakidhi mahitaji kwa asilimia 16.2 ya wakazi wa Mkoa. Takriban asilimia 40 ya eneo la Mkoa halina mtandao wa mabomba ya DAWASA Kiambatisho.
Kutokana na ufinyu wa mtandao, upatikanaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam hautoshelezi mahitaji, huduma ya maji hutolewa kwa maeneo yenye mtandao wa Mabomba. Maeneo machache (20%) yaliyopo hasa katika Wilaya ya Kinondoni, Ilala na Ubungo hupata huduma ya maji kwa saa kati ya 20-24 wakati zaidi ya asilimia 40 hupata maji kwa mgawo wa wastani wa saa kati 8-16 kwa siku.
Takribani asilimia 40 ya eneo la Mkoa halina mtandao wa mabomba ya DAWASA kutokana na uwekezaji mdogo, hivyo kulazimika kutumia visima kama vyanzo vikuu vya huduma ya maji. Wilaya ya Temeke ndiyo yenye kiwango cha chini cha 10% cha upatikanaji wa mtandao wa mabomba ya DAWASA kutokana na kuwa mbali na mtandao wa maji kutoka Ruvu na pia maeneo mengi ni mapya yakiwa ni makazi holela yasiyopimwa na yaliyo pembezoni ambayo yaliendelezwa kuanzia miaka ya 1980.
Mfumo (Central sewerage system) wa kuondosha majitaka uliopo Jijini Dar es salaam unahudumia asilimia 10 tu ya wakazi wote wa Jiji. Mfumo wa Katikati ya Jiji unamwaga maji baharini na mifumo mingine iko Lugalo, Chuo Kikuu cha DSM, Mwenge, Kijitonyama, Mikocheni, Kurasini, Buguruni, Uwanja wa Ndege, Airwing, Barabara ya Nyerere (Tazara), Vingunguti na Ubungo. Mifumo hii inamwaga majitaka katika mabwawa yaliyoko maeneo hayo.
Maeneo yasiyo na mfumo rasmi wanatumia vyoo vya shimo (Pit latrine) na mashimo ya choo (septic tanks) ambapo yakijaa huchukuliwa na kupelekwa kwenye mabwawa kwa ajili ya kusafisha.
Matarajio ya Mkoa ni kutoa huduma ya majisafi na salama kwa asilimia 95 ya wakazi wa Jiji, asilimia 30 uondoshaji wa majitaka na kupunguza upotevu wa maji kwa asilimia 25 katika Mkoa wa DSM ifikapo 2020.
Hivi sasa DAWASA wanatekeleza miradi mikubwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma ya Maji katika Mkoa wa Dar es salaam (Kiambatisho). Miradi hiyo ni pamoja na:-
Lengo la mradi huu ni kuongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 182 hadi 270 kwa siku. Mradi wa upanuzi wa mtambo umekamilika (100%) na umegharimu Tshs billion 66.0. Ujenzi wa bomba kuu kutoka mtambo wa Ruvu Chini pia umekamilika (100%) na umegharimu Tshs bilioni 120.3. Mradi huu umepunguza kero ya maji kwa wakazi wanaotumia maji kutoka mtambo wa Ruvu Chini unaohusisha maeneo ya Bagamoyo na vitongoji vyake, Bunju, Mabwepande, Boko, Tegeta, Kunduchi, Mbezi Beach, Mbezi Juu, Salasala, Kawe, Makongo, Chuo Kikuu, Mikocheni, Msasani, Masaki, Mwananyamala, Kinondoni, Magomeni, Sinza, Manzese, Ubungo, Mabibo, Kigogo, Buguruni, Ilala, Maeneo ya Katikati ya Jiji la DSM pamoja na Kurasini na Bandarini.
Lengo la mradi huu ni kuongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 82 hadi 196 kwa siku ili kukidhi mahitaji hadi mwaka 2032. Ujenzi wa Mradi huu unaendelea vizuri ambapo upanuzi wa mtambo umefikia asilimia 99.8, marekebisho yanaendelea ya kasoro zilizoonekana wakati wa Ukaguzi. Uzalishaji umeanza. Mradi umegharimu ni Tshs 176.4 bilioni. Kukamilika kwa mradi huu kumepunguza kero na uhaba wa maji katika miji ya Mlandizi na Kibaha pamoja na maeneo ya Kiluvya, Kibamba, Changanyikeni, Mbezi, Kimara, Kibangu, Makuburi, Tabata, Segerea, Vingunguti, Airport, Ukonga, Kipawa na Katikati ya Jiji la DSM.
Mradi wa visima virefu 20 Kimbiji na Mpera na Uchimbaji wa Visima vya Majaribio.
Lengo la mradi ni kuzalisha lita milioni 260 za maji kwa siku. Hadi sasa visima 18 vimechimbwa na visima 2 vinaendelea kuchimbwa kati ya visima 20. Utekelezaji wake umefikia asilimia 80. Visima vya maeneo ya Mpera vitahudumia wakazi wa maeneo ya Gongo la Mboto, Chanika, Luzando, Pugu, Mpera, Chamanzi, Kitunda, Ukonga, Kinyerezi, na Uwanja wa Ndege; na visima vya maeneo ya Kimbiji vitahudumia wakazi wa maeneo ya Temeke, Kisarawe, Kibada, Kimbiji, Kigamboni, Tuangoma, Mkuranga, Kongowe, Mbagala, Kurasini, Mtoni, Tandika, Keko na Chang’ombe.
Mradi wa kupunguza upotevu wa maji (Non Revenue Water -NRW)
Mradi huu ni kwa ajili ya kupunguza uvujaji wa maji na maji yasiyolipiwa kutoka asilimia 47 ya sasa hadi asilimia 25 ifikapo mwaka 2020.
Mradi wa Upanuzi wa Mfumo wa Kusambaza majisafi.
Lengo la mradi huu ni kuongeza mfumo wa usambazaji maji na kuunganisha wateja wote walioko katika maeneo yasiyo na mtandao na yale yatakayopata maji kutokana na upanuzi wa mitambo ya Ruvu Chini na Ruvu Juu, pia maeneo yatakayopata maji ya visima vya Kimbiji na Mpera. Mradi huu umeanza kwa baadhi ya maeneo na uko katika awamu kuu mbili ambazo ni:-
Mkataba wa Ujenzi wa Mabomba na Kuunganisha wateja Tegeta hadi Mpiji, Mpiji hadi Bagamoyo na Mbezi hadi Kiluvya. Mradi umeanza kwa ujenzi wa tenki na kituo cha kusukuma maji eneo la Changanyikeni na ulazaji wa mabomba ambapo hadi sasa kazi imefika asilimia 14.4. Kazi hizo zinatarajiwa kukamilika katika mwaka 2017/2018.
Kukamilika kwa mradi huo kutanufaisha Mji wa Bagamoyo na vitongoji vyake, eneo la uwekezaji la Bagamoyo (EPZ), Mpiji, Bunju, Mabwepande, Boko, Mbweni, Tegeta, Ununio, Wazo, Salasala, Kinzudi, Matosa, Mbezi Juu, Goba, Changanyikeni, Makongo, Kiluvya, Kibamba, Mbezi, Msakuzi, Makabe, Malamba mawili na Msigani.
Vilevile, Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia itatekeleza mradi wa ujenzi wa mabomba madogo ya kusambaza maji na kuunganisha wateja katika maeneo ya Changanyikeni hadi Mpiji na Mpiji hadi Bagamoyo. ujenzi utaanza katika mwaka 2017/2018.
Mradi wa Kulaza Mabomba ya Kusambaza Maji Jiji zima kwenye maeneo ambayo hayana mtandao kwa sasa. Mradi huu utahusu ujenzi wa mabomba ya Km 2000 na utaunganisha wateja wapya 500,000. Ripoti ya mwisho na vitabu vya zabuni iliwasilishwa Oktoba 2016. Mazungumzo na Wadau wa Maendeleo yanaendelea kuhusu fedha za kugharamia mradi huu.
Mradi wa Uboreshaji Mfumo wa Uondoaji Majitaka (Upanuzi wa Miundombinu ya majitaka na ujenzi wa mfumo mpya)
Lengo la mradi huu ni kuongeza upatikanaji wa huduma ya Majitaka kwa wakazi wa Jiji la DSM kutoka asilimia 10 ya sasa hadi kufikia asilimia 30 ifikapo Desemba 2017. Kazi ya usanifu wa mradi imekamilika. Kazi zitakazofanyika chini ya Mradi huu ni pamoja na upanuzi wa mfumo wa majitaka katika maeneo ya Katikati ya Jiji, ujenzi wa mfumo mpya Ilala, Magomeni hadi Ubungo, Sinza, Kinondoni, Mwananyamala, Oysterbay, Masaki, Msasani, Kawe, Mbezi Beach, Kurasini, Keko,Chang’ombe na Temeke. Mradi huu pia utahusu ujenzi wa mitambo mitatu ya kisasa ya kusafisha majitaka itakayojengwa katika maeneo ya Jangwani (200,000 m3/siku), Kurasini (11,000 m3/ siku), na Mbezi Beach (16,000 m3/siku).
Benki ya Dunia pia ipi katika hatua za mwisho za kuanza ujenzi wa mifumo 50 ya kusafisha majitaka (DEWATS) katika maeneo mbalimbali ya Jiji. Mradi utaanza mwezi Julai 2017.
Miradi ya visima vya dharura katika maeneo yasiyo na maji ya bomba
Uchimbaji wa visima na ujenzi wa miundombinu katika maeneo yasiyo na maji ya bomba unaendelea. Miradi hii ni hatua ya dharura ili kupunguza kero ya maji wakati miradi mikubwa ya kuongeza maji inaendelea kutekelezwa.
Mkoa wa Dar es Salaam unatekeleza jumla ya miradi 41 ya visima vya maji katika Halmashauri za Manispaa ya Ilala, Kinondoni na Temeke chini ya mpango wa BRN katika sekta ya Maji hususani Maji Vijijini ambayo ni mojawapo ya Sekta 6 zinazotekeleza Mpango wa BRN. Miradi yote iliyokuwa inatekelezwa chini ya Programu ya Maji (RWSP) katika Mkoa wa Dar es salaam iliingizwa katika mpango wa utekelezaji wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Hali ya Utekelezaji wa Miradi hadi Machi 2017.
Chini ya Mpango wa BRN, jumla ya Miradi ya Maji 41 ilikuwa imepangwa kutekelezwa. Hadi Machi 2017 jumla ya miradi 10 ipo kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji ambapo miradi ya Goroka, Kizinga Bughdadi, Mashine ya maji na Mianzini iliyopo katika Manispaa ya Temeke, Kibwegere, Mpijimagohe na Makongo Mbuyuni katika Manispaa ya Kinondoni pamoja na Pugu Kajiungeni katika Manispaa ya Ilala imekamilika na imeshaanza kutoa huduma ya maji. Jumla ya Tshs 6,246,997,666 zitatumika katika ujenzi wa miradi hii kumi kama inavyooneshwa kwenye Jedwali hapo chini.
Jedwali Linaonyesha kwa ufupi maendeleo ya Miradi yote na hatua iliyofikiwa hadi mwezi Desemba 2016.
S/No
|
H/Manispaa
|
Jina la Mradi
|
Utekelezaji (%) |
Gharama ya Mradi.
|
1
|
Ilala
|
Pugu Kajiungeni
|
100 |
862,930,950
|
Kipunguni B
|
99 |
1,319,059,417
|
||
Kivule
|
95 |
852,086,114
|
||
2
|
Kinondoni
|
Kibwegere
|
100 |
479,371,607
|
Mpiji Magohe
|
100 |
341,026,585
|
||
Makongo Mbuyuni
|
100 |
239,907,393
|
||
3
|
Temeke
|
Goroka
|
100 |
587,000,000
|
|
Mianzini
|
100 |
586,615,600
|
|
|
Kizinga Baghdadi
|
100 |
614,600,000
|
|
|
Mashine ya maji
|
100
|
364,400,000
|
|
|
Jumla |
6,246,997,666
|
3.3. Miradi Mingine inayotekelezwa kwenye Halmashauri
Kupitia bajeti za Halmashauri (Own Source, UNICEF, LGCGD, BTC, WATAID, Africa Relief, na mfuko wa Jimbo) Halmashauri zote tano zinaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maji katika maeneo yao kama ifuatavyo:-
Manispaa ya Ilala
Katika Manispaa ya Ilala, jumla ya Miradi 6 katika maeneo ya Pugu Bangulo, Kinyerezi, Bonyokwa, Pugu Kinyamwezi, Pugu Kichangani, Ulongoni A pamoja na Lada ujenzi wake umekamilika na imeanza kutoa huduma kwa wananchi.
Miradi hii ikikamilika yote jumla ya Wananchi 700,703 watafikiwa na huduma ya majisafi na salama katika umbali usiozidi mita 400.
Manispaa ya Kinondoni.
Jumla ya Miradi 4 ya Makongo Juu, Kigogo Buyuni, Makurumla mnara wa Voda na Makurumula sisi kwa sisi imekamilika na inatoa huduma ya maji.
Manispaa ya Temeke
Manispaa ya Temeke, jumla ya Miradi 4 ya Kurasini-Mvinjeni, Buza, Mwasongo-Kisarawe II na Minondo Somangila ujenzi wake umekamilika na imeanza kutoa huduma ya maji. Mradi wa Maji unaohusisha uboreshaji wa huduma ya maji katika kata tatu maeneo ya Kibondemaji umeanza unaotekelezwa kwa msaada wa Shirika la Water Aid umekamilika na umeanza kutoa huduma.
4.0. MAFANIKIO
Kukamilika kwa Mradi Mkubwa wa Ruvu Chini ambao umeongeza upatikanaji wa Maji kutoka Lita Milioni 182 na kufikia lita milioni 270. Mradi umekamilika Mwezi Machi, 2016 na unatoa huduma ya maji kwa Wananchi;
Kukamilika kwa Mradi Mkubwa wa Ruvu Juu ambao umeongeza upatikanaji wa Maji kutoka Lita Milioni 82 na kufikia lita milioni 196. Mradi umekamilika Mwezi Aprili, 2017 na unatoa huduma ya maji kwa Wananchi;
Upotevu wa Maji umepungua (Non Revenue Water) kutoka 47% hadi 38%;
Kukamilika Visima 18 kati Visima 20 vya Kimbiji na Mpera ambavyo vitaongeza upatikanaji wa Maji kwa Lita Milioni 260 ifikapo mwaka 2020;
Kukamilika kwa miradi ya Visima 15 vya ufadhili wa Serikali ya Ubelgiji (BTC) ambayo inahudumia zaidi watu 250,000;
Kukamilika kwa miradi ya visima 8 vya mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Maji (BRN) ambayo inahudumia zaidi watu 120,000;
Matarajio ya Mkoa ni kuwapatia watu huduma ya majisa kwa asilimia 95 ya wakazi wote na uondoshaji wa Majitaka kwa asilimia 30 ifikapo mwezi Desemba 2020.
Changamoto kubwa katika utoaji wa huduma ya maji katika Jiji la Dar es Salaam ni kasi ndogo ya uwekezaji ukilinganishwa na kasi kubwa ya ongezeko la watu. Ongezeko kubwa la watu Jijini hasa kuanzia miaka ya 1980 kwa kiasi kikubwa limechangia katika kuongeza mahitaji ya maji. Serikali kwa kushirikiana na Wadau mbalimbali wanaendelea na juhudi za kutafuta fedha ili kuendeleza miradi ya maji kwa lengo la kukabiliana na mahitaji ya sasa na baadaye. Changamoto zingine ni pamoja na:-
S/NO
|
CHANGAMOTO
|
MIKAKATI
|
---|---|---|
1
|
Kasi ndogo ya uwekezaji ukilinganisha na kasi kubwa ya ongezeko la watu.
|
Upanuzi wa mitambo ya maji Ruvu Juu na Ruvu Chini, uchimbaji wa visima virefu vya maji Kimbiji/Mpera na ujenziwa Bwawa la Kidunda na Upanuzi wa mifumo ya Majitaka
|
2
|
Uhaba wa vyanzo vya maji na umbali vilivyoko unachangia gharama kubwa
ya uendeshaji pamoja na hali ya ukame, uvamizi na uchafuzi wa vyanzo nimambo yanayoathiriuendeshaji wa huduma
|
Kutoa elimu kwa umma na kufanya operation Maalum katika kila Manispaa na kutoa elimu kwa Watendaji wa kata na Madiwani kuhusu ulinzi wa miundombinu ya maji na sheria zake.
|
3
|
Upatikanaji wa maeneo ya
kujenga miundombinu,
|
Kuendelea kuwasiliana na Wadau ili kupata maeneo ya kujenga miundombinu ya maji na pia kutumia way leave zilizopo kwa kukubaliana na Taasisi husika;
|
4
|
Ukuaji na ujenzi holela wa
makazi,
|
Ushirikishwaji wa Jiji, Manispaa na Wizara ya Ardhi katika Upangaji wa Miji.
|
5
|
Wizi wa maji, uharibifu na wizi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka,
unachangia kiwango kikubwa cha maji yasiyolipiwa (zaidi ya asilimia 45) pamoja na uchafuzi wa maji.
|
Kushirikiana na wananchi, vyombo vya ulinzi na usalama katika kulinda miundombinu na kuzuia wizi wa maji na uharibifu wa miundombinu na uchafuzi wa maji.
|
6
|
Watumiaji maji kutokulipa
Ankara za maji kwa wakati,
|
Kuweka dira za maji kwa wateja wote, usomaji wa dira za maji kufanywa kwa kutumia vifaaa maalum vya kuchukua kumbukumbu (data loggers) ili kupata takwimu sahihi.
|
7
|
Gharama kubwa za uendeshaji ikilinganishwa
na makusanyo,
|
Gharama za maji ziende sambamba na Gharama za uzalishaji maji pamoja na uwekezaji;
|
8
|
Mfumo wa kuondoa majitaka haujafika maeneo mengi ya Jiji (unakidhi asilimia 10 tu)
|
|
9
|
Ufinyu wa bajeti ya kutekeleza miradi mipya ya maendeleo na upatikanaji wa fedha za miradi kwawakati;
|
Serikali inaendelea na utafutaji fedha kutoka kwa Wadau wa Maendeleo na kutenga kwenye bajeti kwa ajili ya Utekelezaji miradi mikubwa.
|
10
|
Migogoro ya uendeshaji Miradi ya Maji ya Jamii inayosimamiwa na Jumuia za Watumia Maji (COWSOs).
|
Tathmini imefanyika kuona namna bora ya usimamizi wa miradi ya Jamii. Miradi inayotumia mtandao wa DAWASA na isiyo na utendaji mzuri, uendeshaji wake kuanza kuhamishiwa DAWASCO. Hadi sasa miadi 20 ya Jamii shughuli zake za uendeshaji zimekabidhiwa DAWASCO
|
11
|
Uchimbaji holera wa visima usiozingatia taratibu
|
Kuanzisha utaratibu wa kusajili visima na kutoa vibali. Lengo likiwa ni kupunguza magonjwa yanayosababishwa na maji kutoka kwenye visima visivyo na ubora. Zoezi hili linasimamiwa na Ofisi za Bonde la Wami Ruvu.
|
Tunatoa wito kwa Wadau na watumiaji wa huduma ya maji Mkoa wa DSM kulipia Ankara za maji kwa wakati, kuepuka wizi wa maji na uharibifu wa miundombinu ya maji, kulinda miundombinu iliyopo nainayojengwa ili huduma ya maji iwe endelevu. Aidha, ulinzi shirikishi wa vyanzo vya maji ni budi upewe kipaumbele katika ngazi zote, pia wananchi kutoa taarifaya ya uvujaji wa maji ili kuweza kupunguza upotevu wa maji.
"MAJI NI UHAI NA USAFI WA MAZINGIRA NI UTU"
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Anuani ya Posta: S.L.P. 5429
Simu ya mezani: +255 22 2203158
Simu ya mkononi: +255 22 2203156
Barua pepe: ras@dsm.go.tz
Haki Miliki © 2017 - Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,haki zote zimehifadhiwa